Naibu Waziri wa Kilimo,Mhe.David Silinde afanya ziara Kituo cha Ukaguzi cha Mamlaka Namanga//atoa Maelekezo kwa Wakaguzi

                                         




















 Leo, Agosti 16, 2024, Naibu Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa David Silinde, alifanya ziara ya kukagua shughuli zinazofanywa katika Kituo cha Forodha cha Pamoja (OSBP) kilichoko Namanga, mkoani Arusha. Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Silinde aliongozana na Mkuu wa Wilaya ya Longido, Mheshimiwa Marko Henry Ng'umbi, na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), Prof. Joseph Ndunguru, pamoja na viongozi wengine wa Mamlaka hiyo.

Katika ofisi za Ukaguzi za Mamlaka, Mheshimiwa Silinde alitoa pongezi kwa kazi zinazofanywa na wakaguzi wa Mamlaka waliopo katika ofisi hizo, akisisitiza umuhimu wa kufanya kazi kwa weledi. Alisema kuwa, shughuli hizo ni muhimu sana kwa kuhakikisha kwamba bidhaa zinazopita katika Mpaka huo zinafuata viwango vilivyowekwa, hivyo kusaidia nchi kuepuka kuingiza visumbufu na kuharibu masoko kwa kupeleka bidhaa zisizokidhi vigezo.

Mheshimiwa Silinde alihimiza wafanyakazi wa Mamlaka hiyo kufanya kazi kwa bidii na umakini ili kuongeza mapato kwa nchi na kuhakikisha kwamba bidhaa zinazowasili zina ubora wa hali ya juu. Alisisitiza kwamba, kwa kufanya hivyo, nchi itakuwa na uwezo bora wa kuimarisha sekta ya kilimo na biashara kwa ujumla, hivyo kuchangia katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), Prof. Joseph Ndunguru, alipokea maelekezo ya Naibu Waziri na kuzungumzia umuhimu wa Kituo cha Mamlaka kilichopo katika Kituo Forodha cha Pamoja (OSBP) kilichoko Namanga. Prof. Ndunguru alieleza kuwa kituo hicho ni cha pili kwa ukubwa katika uingizaji wa mapato kati ya vituo 36 vya Mamlaka vya ukaguzi nchini.

Prof. Ndunguru alithibitisha kwamba kituo hiki kina mchango mkubwa katika kuongeza mapato kwa nchi, kutokana na shughuli zake za ukaguzi na usimamizi wa bidhaa zinazopita. Alisisitiza kwamba umuhimu wa kituo hiki hauwezi kupuuziliwa mbali, hasa kwa kuwa kinachangia kwa kiasi kikubwa katika mapato ya serikali.

Aidha, alitoa maelekezo ya kuongeza ufanisi na umakini katika shughuli za ukaguzi ili kuhakikisha kuwa bidhaa zinazowasili zinafaa kulingana na viwango vya afya na usalama. Prof. Ndunguru aliahidi kuendelea kukisimamia vyema kituo hicho ili kuboresha zaidi utendaji wake na kuhakikisha kwamba inatekeleza majukumu yake kwa ufanisi wa hali ya juu.

Comments

Popular posts from this blog

Ni TPHPA tena! yatwaa tuzo Mshindi wa Kwanza

TPHPA WAKABIDHIWA MAABARA YA KISASA ILIYOGHARIMU BIL.3.8, KATIBU MKUU WIZARA YA KILIMO ATOA MAAGIZO

Kanda ya Kaskazini yatolewa kimasomaso na TPHPA Mashindano ya SHIMMUTA 2024//Yatwaa Mataji Matatu huku ikiweka rekodi Maalumu