Wataalamu wa TPHPA Wakutana Kujadili Taratibu za Kufungua Masoko ya Nje kwa Zao la Macadamia
Februari 25, 2025, wataalamu kutoka Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) kutoka idara ya Usimamizi wa Afya ya Mimea walikutana kwa siku tatu katika Ukumbi wa Kituo cha Udhibiti wa Visumbufu vya Mimea Kibiolojia, Kibaha. Lengo kuu la kikao hicho kilikuwa kujadili na kuandaa nyaraka za awali zitakazowezesha kufungua masoko ya nje kwa zao la Macadamia.
Akizungumza na TPHPA Habari, Kaimu Meneja wa Kitengo cha Usimamizi wa Afya ya Mimea, Dkt. Benignus Ngowi, alisema kikao hicho kilijumuisha wataalamu wa masoko ya mazao na afya ya mimea. Waliangazia masuala muhimu kama vile kujua wazalishaji wa zao hilo nchini na kufanya intelijensia kuhusu matakwa ya nchi zinazonunua zao hilo.
Kwa upande mwingine, Kaimu Meneja wa Kitengo cha Malizia Sokoni na Uwezeshaji Biashara, Ndug. Katemani Mdili, alisema mchakato wa kufungua masoko ya nje umeanza kwa haraka kutokana na uhitaji mkubwa wa wakulima wa Tanzania kutaka kusafirisha zao hili kwa ajili ya biashara. Alifafanua kuwa Macadamia ina uhitaji mkubwa duniani, na mnunuzi mkubwa wa zao hilo ni China, inayonunua kwa zaidi ya asilimia 55 ya uzalishaji wa Macadamia duniani, ikifuatiwa na Marekani na nchi za Ulaya. Hata hivyo, alisema kuwa kilo moja ya Macadamia inathamani ya 60,000.
Zao la Macadamia ni fursa kubwa kwa wakulima na uchumi wa Tanzania. Likiwa na thamani ya juu katika soko la kimataifa, macadamia inasaidia kuongeza kipato cha wakulima, kuchochea ajira, na kukuza sekta ya kilimo. Kwa kuzingatia kilimo bora na usindikaji wa zao hili, Tanzania ina uwezo wa kuwa muuzaji mkubwa wa Macadamia duniani.
Comments
Post a Comment